Dhana ya tafsiri na tamthiliya kiswahili


Dhana ya tafsiri na tamthiliya kiswahili:
Mulokozi (1999:188), Anasema kuwa tamthiliya ni fani ya fasihi iliyokusudiwa kutendwa jukwaani kwa ajili ya hadhira fulani
Wamitila,(2003:7) ameeleza kuwa, neno tamthiliya kwa upana wake linatumiwa kujumuisha maneno drama na play kwa kiingera, kwahyo tamthiliya ni utungo unaoandikwa kwa mtindo wa mazungumzo.
Tamthilia ni utungo wa kisanaa ambao huweka wazo fulani katika matendo na mazungumzo (TUKI, 2004).
Hivyo basi tunaweza kusema kuwa tamthilia ni utungo au mchezo wa kuigiza matendo au mawazo fulani yaliyopo katika jamii, ambapo huwa ni majibizano baina ya watu wawili au zaidi.
Catford (1965:20) anasema tafsiri ni kuchukua mawazo yaliyo katika maandishi kutoka lugha moja (lugha chanzi) na kuweka badala yake mawazo yaliyolingana katika lugha nyingine (lugha lengwa).
Mwansoko, (2006) anafasili neno tafsiri ni zoezi la kuhawilisha ujumbe kutoka matini chanzi kwenda matini lengwa.
Hivyo tunaweza kusema kuwa tafsiri ni kitendo cha kufikisha ujumbe wa matini chanzi katika matini lengwa kwa kuzingatia muundo wa lugha lengwa na maana ya lugha lengwa.
Pia tunaweza kusema kuwa tamthiliya tafsiri ni tamthiliya iliyotafsiriwa kutoka lugha moja kwenda lugha nyingine kwa kuzingatia fani na maudhui ya kazi hiyo ya kifasihi.
Kwa mujibu wa Wafula, (1999).Anaeleza kuwa kuna aina nne za tamthiliya zilizo tafsiriwa kama ifuatavyo, kwanza kuna tamthiliya zilizo tafsiriwa kutoka lugha nyingine hadi kiingereza na kisha kutafsiriwa kwa Kiswahili,mfano wa tamthiiya hizo ni pamoja na “MCHUUZI MUUNGWANA” yake Moliere, nyingine ni “MFALME EDIPODE” yake Mbunda Msokile na ile ya “MKAGUZI MKUU WA SERIKALI” yake Nikolai Gogol.
Pia kuna zile tamthilia zilizo andikwa kwa kiingereza na wageni na kutafsiriwa kwa Kiswahili mfano wa tamthilia ilizo tafsiriwa katika mfumo huu ni pamoja na tamthiliya zote za Shake speare.Vilevile kuna tamthiliya zilizoandikwa asilia kwa kiingereza na Waafrika kisha zikatafsiriwa kwa Kiswahili. “MASWAIBU YA NDUGU JERO” na “MZALENDO KIMATHI” ni mifano ya tamthiliya. Kuna tamthilia zilizoandikwa katika lugha nyingine za kiafrika na kutafsiriwa katika Kiswahili mfano wa tamthilia ni “ NITAOLEWA NIKIPENDA”.
Tamthiliya ya Kiswahili ni ile tamthiliya inayojadili mambo mbalimbali yahusuyo utamaduni wa waswahili na iliyoandikwa kwa lugha ya Kiswahili. Mfano; “KAPTULA LA MAKSI” yake Euphrase Kezilahabi na “SAFARI YA CHINGA ”yake Shani Omary.

Zifuatazo ni athari chanja za tamthiliya tafsiri katika tamthiliya ya kiswahili;
 Taaluma ya tafsiri imesaidia kuongezeka kwa machapisho mengi ya kazi za Tamthiliya, hii imefanyika hasa mara baada ya kazi nyingi za tamthiliya kutafsiriwa kutoka lugha nyingine nakutafsiriwa katika lugha ya Kiswahili,mfano wa kazi zilizo tafsiriwa na kuongeza idadi kubwa ya machapisho ni pamoja na “ADUI WA UMMA”,”MKAGUZI WA SERIKALI” na “NITAOLEWA NIKIPENDA”. kazi zote hizi zimesaidia katika kuendeleza ukuaji na kusambaa kwa tamthiliya.
Tafsiri inakuza lugha ya fasihi husika, kupitia tafsiri msamiati mpya unaingia katika lugha husika tukijua kuwa lugha ndio mhimili wa fasihi, kwa hiyo msamiati ukiimarika fasihi pia huimarika.‘Lugha nyingi za kiafrika Kiswahili kikiwa miongoni mwao hazikuwa zimeendelea sana kimaandishi hasa maandishi ya kufasili, kwa hiyo tafsiri za tamthilia zikilenga kukuza maandishi ya lugha za Kiswahili. Na vilevile tamthilia ilitafsiri kwa lengo la kuongeza machapisho ya fasihi ya kiswahili’’ (Ruhumbika 1978).
Tukianza na dhima ya kimaudhui, tumesema kwamba tafsiri imeweza kuibua aina mpya ya maudhui. Hii ina maana kuwa kazi inapotafsiriwa kutoka jamii lugha ambayo imepiga hatua kubwa kimaendeleo kunakuwa na maudhui mapya ambayo yanaweza kuingizwa katika fasihi lengwa hivyo kuweza kuamsha ari ya kimapinduzi. Kwa mfano inapotokea jamii yenye ukandamizaji wa wanawake ila haina mwamko wa kupinga ukandamizaji huo wa wanawake, jamii lengwa huwez kupata mwamko na kujifunza kwamba kukomeshwa kwa ukandamizwaji wa wanawake ni jambo linalowezekana, mfano tamthiliya ya MTAWA MWEUSI.
Kwa upande wa dhima za kifani, tunaona kwamba kazi za tafsiri katika fasihi ya Kiswahili huweza kuibua mitindo mipya ya uandishi. Jamii huweza kutofautiana na huweza pia kuwa na mitindo mbalimbali ya utunzi na uandishi wa kifasihi. Hivyo, kazi ya fasihi inapotafsiriwa kutoka jamii moja kwenda nyingine, jamii lengwa hunufaika na mitindo ya uandishi iliyopo katika jamii chanzi. Katika tafsiri ulingalifu wa mitindo ni jambo la muhimu sana.(Mwansoko na wenzake 2006). Mfano mtindo wa kishairi katika tamthiliya ya MFALME EDIPODE.
Pia tafsiri huweza kusababisha kuingia kwa tanzu mpya katika fasihi lengwa. Kama inavyobainishwa na wataalamu mbalimbali, tanzu za fasihi hutofautiana kutoka jamii moja kwenda nyingine (Samwel 2012, Samwel na wenzake 2013). Hivyo kazi fulani ya fasihi inapotafsiriwa kutoka katika jamii moja kwenda nyingine ambayo haina utanzu husika, jamii lengwa hunufaika kwa kuweza kupata aina mpya ya utanzu. Fasihi ya Kiswahili kwa mfano imenufaishwa sana na utanzu wa tanzia ambao umeingizwa katika fasihi hiyo kutokana na kazi za tafsiri za kifasihi kama vile Oedipus the king (Sophocles ) ambayo imetafsiriwa Kiswahili, MAFLME EDIPODE ((S. Mushi).
Katika dhima ya kutia shime na kuendeleza uandishi wa kifasihi tunaona kuwa tafsiri imeweza kuwatia moyo waandishi na kuweza kuandika zaidi. Mwandishi wa kifasihi anapoona kuwa kazi yake imetafsiriwa katika lugha nyingine na kuoana hadhira pana, hummotisha kutunga zaidi. Aidha kutokea mwandishi akaandika kazi yake ya fasihi na kukosa soko katika jamii aliyoikusudia kutokana na sababu kama vile kukosekana kwa mwamko wa usomaji, umaskini, ukosefu wa elimu na kadhalika. Katika hali kama hiyo, mwandishi husika atanufaika na soko la nje kutokana na tafsiri na hivyo kutokata tama kuandika zaidi. Mfano Ibrahimu hussen katika tamthiliya yake ya KINJEKETILE iliyotafsiriwa kwa kiingereza.
Kupanua hadhira ya kazi ya fasihi. Kazi ya fasihi inapotafsiriwa hupanua hadhira ya kazi ya kifasihi. Kazi hiyo hupata hadhira pana zaidi na hivyo maudhui yake kuwafikia watu wengi zaidi kuliko kama isingetafsiriwa katika lugha nyinginezo. Maudhui ya kazi ya fasihi huwalenga watu hivyo, kama kazi husika itakuwa na hadhira finyu, mchango wa kazi hiyo katika ukombozi wa jamii huwa mdogo pia. Mfano tamthiliya ya NITAOLEWA NIKIPENDA ya Ngugi wa thiong'o.
Tafsiri huongeza msamiati wa lugha. Husemwa kwamba jamii lugha hutofautiana katika mambo mbalimbali ikiwa pia ni utamaduni wa kiwango cha maendeleo kilichofikiwa. Kazi ya fasihi ya jamii iliyopiga hatua kubwa kimaendeleo inapotafsiriwa, huweza kusaidia jamii lugha yenye maendeleo duni kuongeza msamiati. Msamiati wa lugha hutegemeana na kiwango cha maendeleo kilichofikiwa. Lugha ya Kiswahili imenufaika sana na kazi hizi za tafsiri. Pia hudaiwa kuwa lugha kama haitumiki haikui, hivyo kutafsiri kutaifanya lugha itumike hivyo kukua, mfano MFALME EDIPODE, mapebari wa venis.
Tamthiliya tafsiri ni faida inayoongeza hazina ya elimu katika kuzijua jumuiya mbalimbali, na kuzilinganisha na zetu ili kukadiria maendeleo tunayotarajia kisiasa, kijamii na kielimu. Tafsiri kama MABEPARI WAVENISI, JULIASI KAIZARI, MFALME EDIPODE, n.k. zinatekeleza jukumu la kuijenga tamthiliya ya Kiswahili na kupanua viwango vyake kisanaa na kitamaduni.Hivyo basi mbinu hii tafsiri imefanya fasihi ya Kiswahili kukua na kuweza kuendelea kufanyiwa ulinganisho na fasihi nyingine za ulimwengu, mfano: tamthiliya ya “AMEZIDI” ya Said A. Mohamed. Mfano wa kazi zilizotafsiriwa; ALIYEONJA PEPO, NITAOLEWA NIKIPENDA yake ngugi wa thiong’o,” ADUI WA UMMA “na “ORODHA”.Vilevile tafsiri imesaidia kuendeleza fasihi ya Kiswahili na utamaduni wake katika jamii tofautitofauti kwa mfano, kuna kazi za fasihi ya Kiswahili zikiwemo tamthiliya za Kiswahili zilizotafsiriwa ambazo ni pamoja na; “TUFANI” ya Samweli S. Mushi, “SHETANI MSALABANI ”, “MTAWA MWEUSI”na “NITAOLEWA NIKIPENDA” zake Ngugi wa Thiong’o.

MAREJELEO .
Catford J.C (1965). A linguistic translation theory of : An easy in applied linguistics. London: Oxford press.
Method, S.(2015). Umahiri Katika Fasihi ya Kiswahi , Mwongozo Kwa Mwanafunzi na Mwalimu wa Fasihi Simulizi na Andishi. Meveli Publishers (MVP).
Mwansoko H.J.M na wenzake (2006).Kitangulizi cha Tafsiri : Nadharia na mbinu. Dar-es-salaam: TUKI.
Ruhumbika, G. (1978). Tafsiri za kigeni katika ukuzaji wa fasihi ya Kiswahili . Makala.
Wafula, R.M (1999). Uhakiki wa tamtiliya , Historian a maendleo yake . Nairobi Kenya: Jomo Kenyatta Foundation.
TUKI, (2004). Kamusi ya Kiswahil Sanifu. Dar es salaam. Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
Wamitila, K.W. (2003), Kichocheo cha fasihi simulizi na andishi. English press: Nairobi.


Comments

Popular posts from this blog

International Law

KATIBA YA KIKUNDI