Jadili kwa mifano madhubuti majukumu ya fanani na mtambaji na kisha uoneshe mikakati na mbinu za utambaji wa hadithi.



UTANGULIZI,
 Fanani ni mtendaji wa kazi za za sanaa za maonesho. Vilevile fanani ni msani katika fasihi simulizi ambaye anasimulia hadithi, methali, vitendawili, anacheza ngoma na anatumia lugha kueleza dhamira ya kazi yake ya fasihi. Hivyo fanani anaweza kuwa msimulizi kama ilivyo katika ngano, mwimbaji wa nyimbo au manju katika maghani, mtegaji katika vitendawili, mpiga ngoma katika ngomezi au mlumbi katika ulumbi. Fanani aghalabu huwa msimulizi na vilevile mshiriki katika fasihi simulizi (TATAKI  2014). 
Mtambaji ni mtu anayesimulia hadithi au ngano. Vilevile mtambaji ni mtu mwenye tabia ya kujisifu au kwenda mwendo wa matao (TATAKI  2014).  
Mikakati ni mipango maalumu inayoandaliwa kwa ustadi mkubwa ili itumuke kama njia za kufikia malengo Fulani (TATAKI  2014).  
Kwa ujumla tunaweza kusema kuwa fanani ni mtendaji wa kazi za fasihi simulizi mbele ya hadhira yaani kama vile maonesho, masimulizi ya hadithi na kuhusisha matumizi ya lugha za ishara pamoja na miondoko ili kuweza kueleweka kwa hadhira inayosikiliza na kutazama kazi hiyo ya fasihi ana kwa ana.
Yafuatayo ni majukumu ya fanani na mtambaji katika utambaji wa hadithi
Hivyo fanani na mtambaji katika kazi ya fasihi wana majukumu mbalimbali katika utambaji wa hadithi kama ifuatavyo;
Fanani na mtambaji hudumisha na kuendeleza lugha ya jamii yake, kwa mfano kadri fanani na mtambaji wanavyofinyanga lugha ndivyo inavyopevuka na kukua. Fanani na mtambaji hubuni mbinu mbalimbali ya lugha na kuipokeza. Kwa njia hii, lugha hudumishwa na kuendelea kukua zaidi na zaidi  (Wamitila, K. W, 2003)
  Ingawa Fanani katika  ngano si mmoja wapo wa  wahusika wa hadithini, fanani huhusika katika uwasilishaji wa hadithi. Fanani haiwakilishi tu hadithi bali huihusisha na kuifanya kuwa sanaa tendwa pale anapoiwasilisha kwa hadhira hai (Balisidya, N, 1987).
 Katika utegaji wa vitendawili, fanani (mtegaji) huhusika kwa kutega vitendawili, kupokea majibu na kuomba mji baada ya mteguaji (hadhira) kukosa jawabu.
 Fanani hutunga tungo na huzisimulia au kuziwasilisha kwa mfano, anayejigamba hutunga majigambo au vigugo na kuviigiza kwa hadhira hai  (Mulokozi, M.M. 1989).
 Kupitia kwa uwasilishaji wake, fanani hufundisha vijana mbinu za kuiendeleza fasihi simulizi kupitia kwa uwasilishaji wake.
Fanani hutekeleza jukumu la kuelimisha hadhira.Fanani ana jukumu la kuonya, kuarifu, kukashifu, kuelekeza, kufahamisha, kukosoa na  hata kuzindua hadhira yake  (Mulokozi, M.M. 1989).  
 Fanani huendeleza amali na utamaduni wa jamii yake kwa kuupokeza kutoka kizazi kimoja hadi  kingine. Kupitia kwa utambaji na hadhira, kwa mfano, fanani hudhihirisha mazoea ya mtambaji na amali za kijamii zinazofumbatwa na ngano zenyewe kutoka kizazi kimoja hadi kingine  (Wamitila, K. W, 2003)
  Fanani na mtambaji hushirikisha hadhira katika uwasilishaji wake, kwa vile fasihi simulizi ni tendi na ina hadhira hai, ni jukumu la mwakilishaji ( fanani ) kuhakikisha kuwa hadhira yake inashiriki kikamilifu (Wamitila, K. W, 2003)
Vilevile mtambaji na fanani anapaswa kuwa na uwezo wa kuiwasilisha hadithi au ngano kwa namna inayosisimua na kumchangamsha msikilizaji aua hadhira yake. Kufanikisha jambo hili, fanani na mtambaji hawana budi kuwa wabunifu. Ubunifu huu utamwezesha kuiwasilisha ngano ya mapokeo kwa njia inayoipa upya na upekee Fulani kutoka kwa fanani na mtambaji mmoja hadi kwa mwanafasihi mwingine  (Balisidya, N, 1987).
MIKAKATI NA MBINU ZA UTAMBAJI WA HADITHI
Hadithi huwasilishwa kwa hadhira kwa utendaji unaohusishwa na mikakati na mbinu maalumu. Mbinu hizo ndizo misingi maalumu vitambulishi vikuu vya mtambaji wa hadithi. Mbinu zenyewe ni kama zifuatazo;
 Fomula ya utangulizi/ufunguzi, hii ni sifa inayohuiana na uanzaji wa utambaji. Hadithi za mapokeo katika jamii nyingi za kiafrika huwa na utangulizi au fomula Fulani maalumu. Fomula au mtindo huu wa kuanza, mtambaji hurudiwa katika usimulizi wote (Njogu, K. na Chimerah 1999). Jamii ya waswahili, kwa mfano, hutanguliza hadithi zao kwavitangulizi vifuatavyo;
Mtambaji; Paukwa!
Hadhira; Pakawa!     
Mtambaji; Paukwa!
Hadhira; Pakawa!    
           Mtambaji; Hapozamaniza kale………………..

Mtambaji; Hadithi, hadithi!
Hadhira;  Hadithi njoo!
Mtambaji; Hadithi, hadithi!
Hadhira; Hadithi njoo!
                                  
  Mtambaji; Hapozamaniza kale………………..
Fomula za utangulizi hukekeleza majukumu mengine madogo madogo kama yafuatayo:
i) Huwa ni njia ya kuwavuta wasikilizaji pamoja, yaani kuivuta makini ya hadhira inayomsikiliza.
ii) Hutumika kumtambulisha mtambaji wa hadithi.
iii) Huashiria na kuonyesha mwanzo wa adithi.
iv)  Ni njia mojawapo ya kuweka mpaka wa wazi kati ya ulimwengu halisi na ulimwenu wa hadithi.
 Fomula ya Mwisho au fomula-kimalizio, hii ni fomula inayopatikana katika sehemu ya mwisho wa hadithi za kimapokeo katika jamii zilizo nyingi za kiafrika. Jamii nyingi humaliza hadithi zao kwa kimalizio, “Hadithi ( ngano) yangu imekamilika hapo”, “……………………wakakaa raha mustarehe” au “wakaishi raha mustarehe”  (Njogu, K. na Chimerah 1999). Fomula kimalizio hutekelaza majukumu yafuatayo:
i) Huashiria mwisho au kumalizika kwa utambaji.
ii) Huwa ni kama kitangulizi cha shughuli inayofuatia utambaji au utambaji mwingine iwapo pana hadithi nyingine.
iii) Iwapo pana mtambaji mwingine anayefuatia, basi fomula-kimalizio uwa kama kiashirii cha kumwonyeshea kuwa anaweza akaanza.
iv) Huwa ni njia ya kuwapumzisha wasikilizaji au kutuliza hadhira ambayo ilikuwa imetulia na kuwa makini wakati wa usimulizi wa hadithi.
 Virai-kaida, virai-kaida aghalabu huwa ni vifungu vya maneno ambavyo hutanguliza hadithi au simulizi. Virai hivi hupata jina lake kutokana na hali kuwa vinarudiwa na huwa kama kaida Fulani. Mifano ni pamoja na “aliondokeo”, “hapo zamani za kale” na “aliondokea” (Wamitila, K. W, 2003)
             HITIMISHO; Hivyo mtambaji na fanani wana jukumu kubwa sana la utambaji wa hadithi jukwaani kwa kuwa huwa na sifa zinazoubainisha na hadithi zisomwazo vitabuni. Sifa hizi ni sehemu ambayo huipa utambaji utamu usiopatikana tusomapo vitabu na majalida mengine. Hapa hadhira husikia sauti ya mtambaji moja kwa moja. Isitoshe, utambaji na utendaji  wake jukwaani una nafasi kubwa katika kuuwasilisha ujumbe wake mbele ya hadhira. Kwa hiyo, utendaji-simulizi ni utendaji unaotendeka pamoja na lugha. Utamabaji na utendaji huu hujumuisha sifa mbalimbali ikiwemo na matumizi ya usemi halisi, urudiaji, tanakali sauti, matumizi ya viashirii na viashiriaji, kuwepo kwa matendo ya uigaji, mtuo wa kidrama, matumizi ya maleba, uimbaji wa sauti na mambo mengine mengi.



                                                      MAREJEO

Balisidya, N. (1987) “ Tanzu na Fani za Fasihi Simulizi” Katika Mulika Juzuu19. Nairobi University Press.
Mulokozi, M.M. (1989) “ Tanzu za Fasihi Simulizi” Katika Mulika Juzuu 21. Kurasa 1-24.
Njogu, K. na Chimerah (1999) Ufundishaji wa Fasihi: Nadharia na Mbinu. Nairobi: Jomo Kenyatta Foundation.
TATAKI (2014). Kammusi ya Kiswahili sanifu: Toleo la tatu. Dar es salaam: Oxford University Press.
Wamitila, K. W. (2003) Kichocheo cha Fasihi: Simulizi na Andishi. Nairobi: Focus Books.
                             
                                                                                              


Comments

Popular posts from this blog

Historical Background Of Tanzania Revenue Authority (TRA)

It's true that agriculture is a change agent in Tanzania development due to the following reasons;