Jadili wahusika katika riwaya yaMSAKOnaMAKUADI WA SOKO HURIA


CHUO KIKUU CHA STELLA MARIS MTWARA
(chuo kikuu kishiriki cha mtakatifu Agustino)
KITIVO CHA ELIMU
IDARA YA KISWAHILI
KOZI                          :           FASIHI LINGANISHI
MSIMBO                   :           SW 324
MHADHIRI              :            MADAM KANWA 
AINA YA KAZI       :           KAZI YA KIKUNDI
NAMBA YA KUNDI:          NAMBA TANO
JINA LA KIKUNDI            :           SHABAAN ROBERT
WAHUSIKA:           
NA.
JINA LA MWANAFUNZI
JINSIA
NAMBA YA USAJILI
SAHIHI





01.
ABDEREHEMAN MOHAMED R.
ME
STE/BAED/163047

02.
CHACHA ISACK
ME
STE/BAED/ 163031

03
MAZOEA WADI
ME
STE/BAED/162854

04.
MITOTO BAKARI A.
ME
STE/BAED/162893

05.
MOLLEL  LIGHTNESS A.
KE
STE/BAED/162913

06.
MWAYA GOODLUCK J.
ME
STE/BAED/162912

07.
NANYENJE SALUM
ME
STE/BAED/162878

08.
RUKEHA ALESTER
KE
STE/BAED/162929

09.
SARAHAN, JUMA A.
ME
STE/BAED/162819

10.
TEMU JACKSON
ME
STE/BAED/162936


TAREHE YA UWASILISHAJI:  27/5/2019
KAZI; Jadili wahusika katika riwaya yaMSAKOnaMAKUADI WA SOKO HURIA

UTANGULIZI
Muhtasariwa riwaya
MSAKO ni kitabu kilichotungwa na mwandishi maarufu wa Misri Naguib Mahfouz ambaye alizaliwa mwaka 1911-2006 na kutafsiriwa na mwandishi Deogratius M. Simba mwaka 2004 kwa lugha ya Kiswahili na kupigwa chapa na Mkuki na Nyota.
Kama jina la kitabu linavyojidhihirisha MSAKO, ni riwaya inayomuhusu Saber ambaye alikuwa anamsaka baba yake Sayed el Reheimy ambaye hakuwai kumuona tangu kuzaliwa kwake.  Mama yake Saber, Basima Osman anamuagiza Saber kwenda kumtafuta baba yake popote pale ulimwenguni. Katika safari ya msako huo Saber anapitia maisha ya dhiki, chuki, faraja hadi kupelekea kuhukumiwa kunyongwa baada ya kufanya mauaji ya Khalil Abdul Naga ambaye ni mmiliki wa hoteli.
MAKUADI WA SOKO HURIA  ni riwaya iliyoandikwa na hayati Chachage S. Chachage mwaka 1999-2000 na kuchapishwa na E & D Publishers mwaka (2002). MAKUADI WA SOKO HURIA ni riwaya inayochambua na kupembua mfumo wa kisiasa na kiuchumi na mustakabali wa taifa la Tanzania. Ni riwaya ya kihistoria yenye ukweli unaodhihirika leo. inatoa taswira ya mapambano ya watanzania katika kujipatia uhuru na amani ya kweli. Ni mapambano dhidi ya ukoloni na baadae dhidi ya baadhi ya watu walioteka nyara uhuru wa wengi na kushirikiana na wageni kupora rasilimali ya nchi kwa kisingizio cha soko huria. Ni riwaya inayoweka bayana uozo na udhalimu uliojificha katika mfumo wa soko huria ; tamaa, nguvu za uchumi, ubinafsi,  ukandamizaji, Dhuluma,Hujuma, Rushwa Utapeli, Siasa,UkalenaUsasa vimejadiliwa kwa kina katika riwaya hii.      
Wahusika Japhet Lupocho na Mwenerumango wanawakilisha makuadi na wasaliti wengine ambao wameuponda uzalendo wao na kuwa vibaraka wa wawekezaji au wabia.

Dhana ya wahusika
TUKI (1990:169), wamefasili wahusika kuwa ni watu, miti au viumbe vinavyowakilisha watu katika kazi za fasihi. Wahusika hutumiwa katika kazi za fasihi ili kuwakilisha hali halisi ya maisha ya watu katika jamii inayohusika.
Madumulla (2009) akiwarejelea Kasper na Wuckel (1982) anaeleza kuwa, mhusika ni picha ambayo huchorwa na fasihi na ni kiini cha vitu vyote vipya, dhamira na mada katika fasihi. Katika mhusika kuna uwili; mosi, kuna usawili wa kisanaa wa mtu kwa upande mmoja; pili kuna sura ya mtu kwa upande mwingine. Ubunifu wa msanii humuwezesha msanii kuwaumba au kuwasawili wahusika kinafsia, kiakili na kimwili.

 Msokile (1992), akimnukuu Penina Muhando wanasema kwamba wahusika wanaweza kuumbwa kinafsia, kiakili na kimwili. Kutokana na ujenzi wa aina hii, mhusika huonyesha wasifu wake wa ndani na nje au anaweza kuonyesha mabadiliko yake kilaanapokutana na mazingira tofauti. Ataonyesha mabadiliko katika uhalisia wake kwa kuzingatianguvu zinazomzunguka kama vile za utamaduni, siasa, uchumi na kadhalika.

kwa ujumla, wahusika ni nyenzo kuu katika fasihi kwa sababuwahusika ndiyo dira ya matukio na matendo yanayopatikana katika kazi ya kifasihi inayohusika.Mtazamo wa dhana ya wahusika hutofautiana kutegemea mkabala anaouchukua mhakiki nanadharia ya fasihi inayohusika.Mhusika ni mtendaji katika kazi ya kifasihi na huwa kielelezo cha viumbe wanaopatikanaulimwenguni, ingawa si lazima sifa zote za mhusika zifungamane moja kwa moja na zawanadamu.
Aina za Wahusika
Wataalamu mbalimbali wamegawa aina za wahusika kutokana na mitazamo yao. Miongoni mwa wataalamu hao ni pamoja na hawa wafuatao; Ndungo na Mwai, (1991), Msokile (1993) na Wamitila (2002) wameainisha aina tatu za wahusika ambazo ni; wahusika wakuu, wahusika wasaidizi na wahusika wajenzi.
Wahusika Wakuuni wale wanaojitokeza kuanzia mwanzo wa kitabu mpaka mwisho. Hata mara nyingine mhusika mkuu hutumiwa namsanii kama kinywa chake. Yeye ndiye husema nakutenda msanii anayoyapendelea yaeleweke katika jamii.
Wahusika Wadogo (Wasaidizi) ambao wanaomzingira mhusika mkuu na wanaomsukuma aamue au asiamue jambo kinyume chake. Wahusika hawa hujitokeza hapa na pale katika kazi ya fasihi. Wahusika wadogo husaidia kuijenga dhamira fulani inayojadiliwa katika kazi ya fasihi.
Wahusika Wajenzi, niwahusika ambao kwa kiasi kikubwa hutumika kwa lengo la kujenga au kukamilisha Maudhui ya kazi ya mwandishi. Pia hutumika kushirikiana nawahusika wakuu na wahusika wasaidizi

Kwa mujibu waNjogu na Chimerah (1999) wameainisha aina kuu nne za wahusika ambao ni; Muhusika Mkwezwa, muhusika wa kisaikolojia, muhusika wa kimapinduzi na mhusika jumui. Mhusika mkwezwanimuhusika mwenye sifa za kiutendaji. Ni hodari na shujaa kama wahusika wa fasihi simulizi.
Muhusika wa Kisaikolojia; Huyu ni muhusika anayekumbana na matatizo mengi ya kijamii na anaibusha hisia za huruma kwa wasomaji.
Muhusika wa Kimapinduzi; huyu ni muhusika anayeelewa historia, siasa, mazingira na hali ya kiuchumi ya jamii yake. Yuko radhi kujitoa muhanga kubadilisha maisha ya wanyonge. Ana itikadi kali na msimamo thabiti.
Muhusika Jumui; Ni muhusika wengi katika mmoja.Hupatikana zaidi katika fasihi ya kidhanaishi. Muhusika huyo mmoja anakuwa na sifa za wahusika wengi. Anatumiwa kuonesha fujo za maisha. Hivyo anaitwa muhusika jumui. Mfano muhimu ni “mimi” na “sisi”.

Wahusika katika riwaya teule; MSAKO na MAKUADI WA SOKO HURIA
Katika kujadili suala la wahusika waliojitokeza katika riwaya hizo teule tunarejelea nadharia ya uhalisia kama mwongozo wa mjadala huu.
Nadharia ya Uhalisia
Kwa mujibu wa Wamitila (2000), nadharia ya uhalisia ni mojawapo ya matapo maarufu katika ulimwengu wa fasihi na lenye athari kubwa sana. Dhana ya uhalisia hutumiwa kwa maana mbili kuu. Maana hizo ni kuelezea tapo la kipindi maalum katika fasihi na kuelezea aina ya mtazamo au tapo la kifasihi ambapo kazi za fasihi zinachukuliwa kama zinavyohifadhi au kuakisi sifa za kimsingi zinazohusishwa na uhalisi. Uchunguzi wa utanzu unaoambatana na uhalisi kwa kiasi kikubwa hauwezi kuzungumzia riwaya bila ya kuyarejelea mawazo yanayohusisha uhalisia. Wanauhalisia hufanya hivi ili kujifunga kwenye wahusika wa kawaida au wanaoweza kupatikana katika jamii halisi. Kuyachunguza na kuyasimulia maisha yao na tajriba zao na kusawiri kwa kuonesha mandhari na mazingira ya kawaida.

Tapo hili limewekewa msingi na mwanafalsafa anaejulikanwa kama Hegel (1995) katika kitabu chake Aesthetik (ujumi).  Kuna faida kubwa tatu zinazopatikana katika matumizi ya tapo hili. Kwanza, ni kusisitiza uainishaji wa maisha ya jamii kupita wahusika kwa uaminifu mkubwa. Pili, mtazamo huu unatia mkazo kwenye uwasilishaji kwa mambo ambayo yanaonekana katika jamii inayohusika, na tatu hutoa nafasi ya kuyasawiri matukio, mandhari na wahusika ambao huwenda wasiafikiane au wawafikiane na uhalisi wa jamii yake.

Kwa kumrejelea Wamitila (2002:21), tunajadili baadhi ya wahusika waliojitokeza katika riwayahizi kama ifuatavyo; Tukianza na riwaya ya MSAKO.
SABER, Huyu ni mhusika mkuu ambaye habadiliki na hakui kisaoikolojia. Hii ni kutokana na matendo yake na tabia zake kutobadilika. Mwandishi amemchora mhusika huyu Kama; muuaji, mwizi, mhalifu, hana mapenzi ya kweli, ni malaya na mhuni. Mwandishi hakuonyesha mabadiliko yoyote ya tabia ya mhusika huyu. Mwandishi amemchora Saber kama mhusika mkuu ili kuonyesha kuwa katika jamii zetu kuna watu wasiobadilika. Hafai kuigwa na jamii
SAYED SAYED EL-REHEIMY; mhusika huyu amechorwa kama mhusika mjenzi. Huyu ndiye baba yake Saber.Yaani amepewa sifa na uwezo uliopitiliza ukilinganisha na uhalisi wa maisha yake yalivyo. Amechorwa kama mtu maarufu, mpenda starehe, tajiri na mwenye hadhi. Mfano (uk9) mwandishi anaeleza sifa za muhusika huyu. Mhusika huyu amechorwa kama mtu wa tabaka la juu kwani amekuwa mwakilishi wa tabaka la wenye nacho, pia, kama mtu mbinafsi kulingna na tabia zake alizokuwa anafanya.
“Yeye ni mtu mwenye kipato kizuri kabisa. Wakati huo alikuwa mwanafunzi bado, lakini hata wakati huo alikuwa na uwezo wa kutosha na hadhi.”
Mhusika huyu hafai kuigwa na jamii kutokana na tabia zake.
SHEHE, Ni mhusika ambaye pia tumemfahamu kwa kusimuliwa (maizi), hivyo ni mhusika mjenzi ambaye amewakilishwa dhahili, pia mhusika tunamtazama kama mtu anayewakilisha tabaka la wanadini, kwani anawakilisha kundi la watu wanaoamini dini na watu wanaoabudu. Mfano
 “Shehe ambaye alikuwa ameketi huku amekunja miguu akiwa katika tafakuri nzito, alisema, “tafuta na utapata.”(uk16)
Ni kielelezo bora kwa jamii kutokana na kuwakilisha kundi la wanadini wenye imani ya kweli. Hivyo anafaaa kuigwa katika jamii.
BWANA KHALIL ABDUL NAGA, Huyu ni muhusika msaidizi ambaye huwa anakua kiakili na anabadilikabadilika na ana sifa za uzuri na ubaya. Mhusika huyu tunamtazama kama mtu wa tabaka la juu kwani anawakilisha tabaka la watu wenye kipato yaani matajiri na yeye ni miongoni mwa matajiri wa jijini Cairo. Mhusika huyu ni mmiliki wa Hotel ya Cairo, ni mme wa Karima, ni mzee kiumri, ameuawa na Saber. Kwa kiasi fulani anafaa kuigwa na jamii kwa kuweza kuajiri watu wenye kipato cha chini ili kuwainua kiuchumi. Kwa upande mwingine hafai kuigwa kwa tabia ya kutimia mali zake kuwaoa mabinti wenye umri mdogo kama Karima.
ALY SERIAKOUS, Huyuni mhusika msaidizi, ni kijana mwenye tabia nzuri, vilevile ni mhusika ambaye amewakilisha tabaka la watu wenye kipato cha chini na wenye kuhangaika na vibarua kila siku. Ni mchukuzi katika Hotel ya Cairo, ni kibarua wa Khalil, alihusishwa na kifo cha Khalil, ni kijana mchangamfu na mchapakazi, pia amesingiziwa kesi ya mauaji. Kwa kiasi kikubwa anafaa kuigwa katika jamii kwani ni mhusika ambaye anapenda kuwasaidia watu.
ELHAM, Ni mwanamke mchapa kazi na anafanya kazi katika ofisi za gazeti la sphinx na ana sifa ya upole na mwenye huruma. Mchumba wa Saber, hamjui baba yake, ni mwanamke msomi na anayejitambua, ana mapenzi ya kweli, ni mwanamke mwenye msimamo. pia mhusika tunamtazama kama mfanyakazi anayependa kufanya kazi kwa bidii. Kutokana na tabia ya mhusika huyu anafaa kuigwa katika jamii yetu ya leo.
KARIMA, Ni mke wa Khalil, mwanamke asiye na huruma (mkatili) na ni msailiti, ambaye mali zote za Khalil zipo chini yake. Tunaona kuwa ni miongoni mwa wauaji wa bwana khalil na mwenye tamaa ya mali. Pia ni mhanga wa mila potofu, kwani aliolewa na mwanaume asiyempenda kwa sababu ya umaskini na tamaa za pesa.Hivyo ni mhusikaambaye tunamtazama kama mtu mbinafsi. Hafai kuigwa katika jamii kwani ni kiwakilishi cha watu ambao hawana utu.
Pia katika kitabu cha MAKUADI WA SOKO HURIA mwandishi amejadili wahusika na sifa zao katika riwaya hii kama ifuatuatavyo;
Binti Wenga, huyu ni mhusika mkuu katika riwaya hii, ni mhusika ambaye anawakilisha vyema nafasi ya mwanamke aliye shupavu na mpenda maendeleo. Binti wenga siyo mtu mashuhuri katika mambo ya siasa, Mama huyu hana ubinafsi bali anatumia uwezo wake katika kutetea haki za nchi yake na wananchi kwa ujumla
            Alikuwa ni mwanamke aliyeshuhudia ukombozi mpya, aliheshimiwa na wanawake wote na kuhofiwa na wanume wa pale kijijini….(uk 111)”
Binti wenga ni kielelezo cha wanamama wengi mahodari na majasiri katika jamii yetu, hivyo anafaa kuigwa katika jamii.
Njovu Luhala;ni mhusika msaidiziambaye amejadiliwa kwa kuwa na sifa ya kutetea tabaka la wawekezaji ambao wananyonya wanyonge au wananchi kwa kuchukua maeneo na aridhi zao bila malipo yoyote,Mbunge Luhala ni mwakilishi wa viongozi wa ngazi ya juu wanaowakandamiza wananchi na kuwapora haki zao kwa kuwa na miradi kama ule wa ufugaji wa kamba katika bonde la Rufiji, ambao haukuwa na budi kumilikiwa na kuendeshwa na Wanarufiji wenyewe. Ni kielelezo cha viongozi wengine wengi katika jamii ambao wanatumia madaraka yao kuwakandamiza wengine, kwani anadiriki hata kumpa ujauzito binti mdogo akiwa katika majukumu yake ya kazi huko bungeni, hivyo hafai kuigwa katika jamii yetu ya sasa.
Fidelis Mvumi Msakapanofu; ni mhusika mkuu ambaye ni mwandishi wa habari pia ni msimulizi anayesimulia hadithi ya riwaya nzima kwa kutumia nafsi yakwanza. Mhusika huyu ni mpambanaji na mpenda haki ambaye anapambana kuweza kufichua mabaya yaliyo jificha juu ya wananchi wa Rufiji ambao wana dhulumiwa ardhi na mabeparia wa kigeni kutokana na mfumo  hasi wa soko huria unaowakandamiza wananchi na kuwanyima haki zao. Pia mhusika huyu anaenda kujuana na ndugu au ukoo wake huko Rufiji baada ya kutengana nao kwa mda mrefu bila kuonana. Kutokana na tabia njema ya kutetea haki ya wanyonge, anawakilisha tabaka la watu wema katika jamii, hivyo anafaa kuigwa katika jamii.
Bwana Nyakilanzi;ni mhusika msaidizi ambaye ni mwenyekiti katika kijiji cha Nyamisati ni kiongozi bora anayependa maendeleo, kwani anawashilikisha wanakijiji wake katika kufanya maamuzi na kupanga mipango na kuitekeleza kwa maslahi ya umma. Anakuwa mstari wa mbele katika majukumu yote pale kijijini. Hana ubinafsi, na kwa misingi hii huwa ni mtu wawatu mwenye kutetea wanyonge na haki zao katika jamii yake, hata katika jamii yetu ya leo watu kama hawa wanopenda utu na Amani wapo. Mhusika huyu ni kielelezo cha viongozi wapenda maendeleo na watetea haki za wanyonge katika jamii, hivyo anafaa kuigwa katika jamii.
Alhaji Seif Said;ni mhusika msaidizi ambaye anaonekana mwanzoni kuwa na msimamo wa kutaka kuisaidia nchi yake kuondokana na unyonyajia na suala la ufisadi. Ni mwandishi wa habari ambaye alifichua suala la uwepo wa mahindi huko Ruvuma, pia aliandika kuhusu jinsi viongozi walivyo itelekeza meli ya India na bei ya ununuzi kuhusu zao la korosho Mtwara na Lindi. hali iliyopelekea kupewa onyo kali na kuteuliwa kuwa msajiri wa magazeti mwishoni mwa miaka ya themanini. Pia anakataa kusajili gazeti la Fidelis ambaye alikuwa akiandika na kusuta juu ya mambo mabaya yanayofanywa na baadhi ya viongozi wa serikali.
Lazima litafungiwa. Haritarusiwa. Na mimi nitahatarisha wadhifa wangu… (uk 18)”
Japhet Lupocho na Mwenerumango; wanawakilisha makuadi na wasaliti, ni waponda uzalendo wa nchi yao na kuwa vibaraka wa wawekezaji, ni matajiri uchwara ambao wanakubali kurubuniwa na mwekezaji mwingereza Paul Mooney kwamanufaa yao binafsi. Hawa ni kielelezo cha matajiri wanaohujumu uchumi wa nchi hivyo kwa kiasi kikubwa hawafai kuigwa katika jamii.
Paul Mooney na Balfour Beatty; wawekezaji mashuhuri nchini ambao wanatumia uwezo wao wa kifedha kuteka mawazo ya Japhet Lupocho na Mwenerumango na hatimaye wanakuwa wasemaji wa mwisho na kunyonya rasilimali za watanzania na kuwacha wananchi wakiwa masikini, hivyo hawafai kuigwa na jamii.
Sifunina Mjuba; ni wanaharakati wenye msimamo wa kimapinduzi. Kwa sababu ya kunusuru uuzwaji wa Delta ya Rufiji wanatekwa na Kaboko, Mayasa na Willy. Ni wapenda maendeleo na wanafaa kuigwa katika jamii. “…wale waandishi wa habari walio nusuru taifa hili na janga la uuzwaji wa Delta ya Rufiji kwa matapeli”
Oscar Mayowe; ni mwandishi wa magazeti, ni msaliti na asiye na upendo wa dhati. anampa mimba binti waziri, anakubali kuvunja uhusiano na mkewe ili amuoe binti waziri. Kutokana na tabia yake ya usaliti hafai kuigwa katika jamii. “Ndoa mahususi ya kiislamu inatarajiwa kufanyika mwezi wa tatu”.
HITIMISHO
Pamoja na kwamba waandishi wa riwaya hizi wana asili tofauti lakini bado kazi zao zina mfanano mkubwa kuliko kutofautianaRiwaya hizi za MSAKO na MAKUADI WA SOKO HURIA ni riwaya zinazosawili mazingira halisi ya jamii za nchi zinazoendelea barani Afrika. Kwa mfano waandishi wa vitabuu vyote wamewatumia waandishi wa habari ikiwa kama ni njia ya kutatua matatizo yanayoikabili jamii husika; mwandishi amemtumia mhusika Elham na Tantawi katika kitabu cha MSAKO kutoa msaada wa kumtafuta baba wa Saber, lakini pia mwandishi amewatumia wahusika kama vile Fidelis, Sifuni, Mjuba, na wengine kuyasemea yale maovu yote yaliyotokea katika jamii ya watanzania.
Katika suala la kutofautiana kwa wahusika wa riwaya hizi mbili tunaona kwamba, kwa kiasi fulani riwaya hizi zinatofautiana, tukianza na waandishi wenyewe tunagundua kuwa Naguib Mahfouz ni mzaliwa wa Misri na kwa upande wa Chachage S. Chachage ni mzaliwa wa Tanzania hivyo wanatoka katika tamaduni tofauti. Lakini hata pia kupitia wahusika tunagundua kwamba riwaya ya MAKUADI WA SOKO HURIA imejikita katika kufanya mapinduzi ya watanzania kujikomboa na udhalimu wa kipebari, wakati riwaya ya MSAKO imejikita katika msako wa Saber kama jina la kitabu linavyodokeza.
Kupitia dhana ya wahusika waandishi wameweza kuwachora wahusika katika namna mbili, wale wafaao kuigwa na wale wasiofaa kuigwa kutokana na matendo na tabia zao. Hivyo kupitia wahusika, jamii inaweza kubadilika kimtazamo chanya au hasi kwa kuwa kazi ya fasihi lazima iache athari katika jamii husika.

MAREJEO
Chachage, Chachage Seithy L. (2002). Makuadi wa Soko Huria. Dar es Salaam: E & D Publishers            Limited
Madumulla, J. S (2009). Riwaya ya Kiswahili. Dar-es-salaam: Mture Educational Publishers
Mahfouz, N (2004). Msako. Dar-es-salaam: Mkuki na Nyota Publisher
Msokile, M. (1992). Kunga za Fasihi na Lugha. Dar-es-salaam: Educational Publishers and            Distributors Ltd
Njogu, K. na Chimerah, R. (1999). Ufundishaji wa Fasihi Nadharia na Mbinu. Nairobi: Jomo        Kenyatta Foundation Ltd
Ndugo, C. M na Mwai W. (1991). Historical and Modern Development of Kiswahili. Nairobi       University Press. Nairobi
TUKI, (1990). Kamusi Sanifu ya Isimu na Lugha. Taasisi ya uchunguzi Tanzania. Dar-es-salaam:  Chuo Kikuu   
Wamitila, K. W. (2002). Uhakiki wa Fasihi Msingi na Vipengele Vyake. Phoenix Publisher Ltd


Comments

Popular posts from this blog

International Law

KATIBA YA KIKUNDI