Makala

 

Makala hii imegawanyika katika sehemu tatu, Yaani utangulizi, kiini na mwisho.

 Utanfulizi wa kazi tumejadili:

a)maana ya muundo,

b)maana ya sarufi miundo kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali,

c)maana ya jumla ya sarufi miundo,

d)waasisi wa sarufi miundo

e )malengo ya sarufi miundo,

 kiini cha kazi  tumejadili utengamano wa sarufi miundo na matawi mengine ya sarufi kama vile;

a)fonolojia na sarufi miundo,

b)mofolojia na sarufi miundo

c) semantiki na sarufi miundo

 mwisho

hapa tumehitimisha kazi yetu.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

      Kabla ya kueleza maana ya Sarufi miundo, tufafanue kwanza dhana ya muundo. Muundo ni mpangilio wa vitu vidogo vilivyowekwa pamoja na kujenga kitu kikubwa zaidi. Kutokana na fasili hii ya muundo twaweza kuihusisha na lugha kuwa nayo huundwa na vipashio vidogo ambavyo huwekwa pamoja

     Sarufi miundo au sintaksia ni tawi la isimu ambalo linahusu namna maneno yanavyoungana na kuhusiana katika kirai au sentensi. Sintaksia inachunguza namna maneno yanavyojipanga katika sentensi kwa kuzingatia kanuni za Sarufi ya lugha husika. Huu ni mkabala wa kuchunguza vipashio vya lugha vinavyoungana na kujenga vipashio vikubwa zaidi. Katika uchambuzi huu huonesha uhusiano baina ya maneno katika sentensi na kanuni za kuyapanga maneno hayo katika tungo hata yakaleta maana. Katika mpangilio huu kuna maneno ambayo lazima yatangulie au yafuate maneno mengine. Aidha katika kuchunguza jinsi maneno yalivyopangwa katika tungo, tunachunguza pia jinsi maneno yanayofuatana yanavyohusiana. Sarufi miundo au sintaksia inahusu maneno pamoja na viambishi vyake na namna yanavyoungana na kuunda kirai na sentensi

    Mkabala wa Sarufi miundo uliasisiwa tangu karne ya 19 na wanaisimu wa Ulaya k.v. Frednand de Saussure (1857-1913) na Mmarekani Leonard Bloomfield (1887-1949) na baadaye Noam Chomsky ambaye alileta mabadiliko makubwa katika mkabala huu

 

   Besha (1994),anaifasili sarufi miundo au sintaksia kua ni taaluma inayojihusisha na uchambuzi na ufafanuzi wa muundo wa sentensi za lugha; kwa mujibu wa O’Grady (1996), sintaksia ni taaluma inayochunguza jinsi maneno yanavyounganishwa ili kuunda sentensi.     

 

    Sintaksia kwa mujibu wa Massamba na wenzake (2009)wao wamifasili sntaksia kua ni utanzu wa sarufi unaojishughulisha na uchanganuzi wa mpangilio wa maneno katika sentensi na uhusiano wa vipashio vyake. Wanaendelea kusema kuwa katika utanzu huu kinachochunguzwa ni zile sheria au kanuni ambazo hazina budi kufuatwa katika kuyapanga maneno ya lugha katika mfuatano (neno moja baada ya jingine) kwa namna ambayo itayafanya maneno hayo yalete maana inayokubalika na kueleweka katika lugha husika.

       Fasili hizi chache tumezitoa kama mifano tu ya kushadidia hoja ya kwamba kuna fasili nyingi za sintaksia. Pamoja na kuwapo kwa fasili nyingi, mtu akichunguza atagundua kwamba fasili takriban zote zinabainisha kuwa sintaksia ni tawi la isimu linalojihusisha na uchunguzi wa:

      (a) Jinsi maneno yanavyopangwa katika tungo

       (b) Kanuni au taratibu za lugha zinazotumika na zinavyotumika katika kuyaweka maneno hayo pamoja Kwa hiyo, sintaksia inaweza kufasiliwa kuwa ni taaluma inayochunguza miundo ya tungo na kanuni mbalimbali za lugha zinazotawala miundo hiyo. Katika uchunguzi huo, sintaksia huhusika na mpangilio wa maneno katika miundo mitatu iliyopangwa kidarajia, yaani jinsi maneno yanavyopangwa ili kuunda virai, vishazi na sentensi.

Kabla ya kuangalia utamano wa sarufi miundo na matawi mengingine ya sintaksia tunaanza kwa kuyabainnisha matawi hayo sambamba na fasili zake kamaifuatavyo;

Fonetiki

         Massamba na wenzake (2004) wanaeleza kuwa fonetiki ni tawi ambalo hujishughulisha na uchambuzi wa taratibu zote zinazohusiana na utoaji, utamkaji, usafirishaji, usikiaji na ufasili wa sauti za lugha za binadamu kwa ujumla. Kinachozingatiwa hapa ni kuchunguza maumbo mbalimbali ya sauti zinazoweza kutolewa na ala sauti, namna ambavyo maumbo hayo yanavyoweza kutolewa, yanavyoweza kumfikia msikilizaji (yaani yanavyosikika) na yanavyofasiliwa na ubongo; bila kujali sauti hizo zinatumika katika lugha gani. Kwa kusikiliza sauti wanafonetiki wanaweza kuzipanga sauti hizo katika makundi na kuzitolea sifa zinazotofautisha sauti moja na nyingine.

      Fonetiki ina matawi kadhaa kama Vile:  Fonetiki Matamshi, FonetikiAkustika, Fonetiki Masikilizi/Masikizi na Fonetiki Tiba matamshi.

 

Fonolojia

    Fonolojia ni taaluma inayotafiti ili kujua jinsi sauti za lugha zinavyofanya kazi katika lugha husika kama chombo cha mawasiliano katika jamii husika.

 

 Mofolojia

      Mofolojia ni tawi la isimu ambalo huchunguza muundo wa neno kwa kubainisha viambajengo vinavyounda umbo hili. Kwa kuwa neno huundwa na mofu, uchambuzi wa viambajengo vya neno hubainisha mofu zinazounda neno, aina zake na jinsi zinavyoungana na kuunda neno lenye maana. (TUKI 199O)

 Mgullu (1999).anasema kwamba mofolojia ni taaluma inayoshughulikia si tu vipashio vya lugha vinavyoliunda neno la lugha hiyo, bali pia minyambuliko ya maneno yaliyoundwa kwa vipashio husika ambavyo wanaisimu huviita mofu.

Semantiki

      Awali neno semantiki lilitumika kumaanisha sayansi ya “maana” kwa ujumla, hivi kwamba ilishughulikiwa na wanafilosofia, wanasaikolojia, wanamantiki, wanaanthropolojia na wengineo. Baadaye stadi hii ilijishughulisha zaidi na maana katika muktadha wa mwanadamu. Dhana ya maana ni dhana ya kidhahania, hivyo wataalamu wa isimu wamejaribu kueleza dhana hii kiutendaji. Kiutendaji maana inaweza kubainishwa katika kiwango cha neno na kiwango cha tungo/sentensi.

       Habwe na Karanja wakimnukuu Richard na Wenzake (1985) wanasema “Semantiki ni stadi ya maana. Semantiki ni utanzu unaochunguza maana katika lugha ya mwandamu”. Wanaendelea kusema semantiki hutafiti maana za fonimu, mofimu, maneno na tungo

Nadharia ya Sintaksia ambayo mwasisi wake ni Noam Chomsky imejaribu kueleza vipengele vya kisintaksia vya lugha mbalimbali ili kuonyesha jinsi lugha mahsusi zinavyopanga maneno yao ili kupata sentensi.

Lengo la Chomsky katika uchanganuzi wake wa lugha ni kuunda nadharia ya sintaksia ya jumla itakayoonyesha vipengele vya kisintaksia vinavyopatikana

katika kila lugha na jinsi vinavyotofautiana. Hii inafahamika kama nadharia

ya sarufi ya jumla.

Lengo lingine la Chomsky ni kupinga mtazamo wa wanaisimu wa miaka 1950 (wanamapokeo) waliodai kuwa tofauti za lugha hazina ukomo, mtazamo ambao hakuuafiki kwani ulimaanisha kuwa ingebidi kila lugha iwe na nadharia yake. Alidai kuwa tofauti baina ya lugha ni ndogo na kwamba

nadharia ya sarufi ya lugha ingeweza kujumuisha lugha zote isipokuwa kwa tofauti ndogondogo tu. Alibainisha kategoria za virai kuwa ni:

 KN,  KT,  KV,  KE,  KH,  KU.

      Baada ya kutazama matawi ya isimu na ufafanuzi wake sasa tutazame utangamano kati ya sarufi miundo na matawi mengine ya sintaksia yaani fonolojia, mofolojia na semantiki kama ifuatayo ;

      Uhusisno uliopo kati ya sintaksia na fonolojia

Massamba na wenzake (1999) wanasema fonolojia ni uchambuzi wa mfumo wa sauti katika lugha mahususi kwamaana ya jinsi ambavyo vitamkwa au sauti za lugha zinavyoungana ili kujenga maneno katika lugha. Ni dhahiri kwamba kuna uhusiano usio na mashaka kati ya sintaksia na fonolojia kwa sababu hatuwezi kuwa na miuundo mikubwa bila kuwa na mpangilio sahihi wa sauti katika lugha.

Mfano 1. ‘anacheza’ hili ni neno lakini pia ni sentensi, hivyo linaweza kuchanganuliwa kifonolojia kama, /a/n/a/ch/e/z/a/. kwa hiyo mpangilio sahihi wa sauti hizo ndizo zinazounda neno ‘anacheza’.

Mfano 2 (a). neno “debe” neno hili limeundwa na konsonanti irabu konsonanti irabu (KIKI).

           2. (b). “edbe” hili limeundwa na irabu konsonanti konsonanti irabu (IKKI).

Katika mfano 2a, neno “debe” lina maana na limefuata kanuni na mpangilio unaokubalika katika lugha ya Kiswahili, lakini katika mfano 2b neno “edbe” halina maana katika lugha ya Kiswahili kwa sababu halina mpangilio sahihi wa vitamkwa au fonimu.

Kwa hiyo mpangilio sahihi wa sauti katika maneno ndio husaidia kupata vipashio vikubwa zaidi katika lugha kama vile kirai, kishazi na sentnsi. Kwa hiyo kuna utangamano kati ya sintaksia na fonolojia kama inavyoonekana katika mfano wa 2a na 2b

      Uhusiano uliopo kati sintaksia na mofolojia.

Besha (2007:49) anasema “mofolojia ni taaluma inayojishughulisha na kuchambua muundo wa maneno katika lugha’.Pia Rubanza (1996:1) anasema “mofolojia ni taaluma inayoshughulikia vipashio vya lugha katika kuunda maneno”. Maumbo ya kimofolojia huathiri vipengele vingine vya kisintaksia kama vile kipengele cha umoja na wingi, katika maumbo ya kimofolojia ndicho kinachoathiri umbo linalofuata jina na kuathiri muundo wa sentensi nzima. Kwa mfano,

                       Mfano 3a,  Mtoto alikuwa anajifunza kusoma.

                       Mfano 3b,  Watoto walikuwa wanajifunza kusoma.

Katika mifano hii kiambishi m- na wa-katika upande wa kiima vimeathiri utokeaji wa viambishi a- na wa- katika upande wa kiarifu. Hivyo taaluma ya sintaksia na mofolojia haziwezi kutenganishwa.

Kwa ujumla sintaksia kama tawi mojawapo la isimu linauhusiano wa moja kwa moja na matawi mengine kwani haiwezi kutenganishwa na vitengo vingine vya lugha kutokana na uhusiano mkubwa uliopo baina ya vitengo hivi. Hutegemeana na kuathiriana kwa kiasi kikubwa, mfano huwezi kupata mofolojia bila kupitia ngazi ya fonolojia pia huwezi kuwa na ngazi ya sintaksia bila kupitia ngazi ya fonolojia na mofolojia .

Uhusiano uliopo kati ya sintaksia na semantiki.

        Habwe na Karanja wakimnukuu Richard na Wenzake (1985) wanasema “Semantiki ni stadi ya maana. Semantiki ni utanzu unaochunguza maana katika lugha ya mwandamu”. Wanaendelea kusema semantiki hutafiti maana za fonimu, mofimu, maneno na tungo. Hivyo kutokana na fasili hii maana hushughulikiwa katika vitengo au viwango vyote vya lugha ambavyo ni fonolojia, mofolojia na sintaksia. Kwa mfano,4

    Mfano 4a;   Mtoto mtiifu amefaulu mtihani.

          Mfano 4b;   Mtihani mtoto amefaulu mtiifu.

          Mfano 4c;   Mtiifu mtoto mtihani amefaulu.

Katika mifano hii sentensi (4a) ina maana kwasababu imefuata mpangilio sahihi wa maneno katika tungo na sentesi zilizobaki hazina maana kwasababu hazijafuata mpangilio sahihi wa kimuundo katika lugha . Kwa mantiki hii, semantiki hushughulikia viwango vyote vya lugha, hivyo hushughulikia pia kiwango cha sintaksia ambapo huangalia maana za tungo, kwani tungo lazima ikubalike kwa wazungumzaji wa lugha husika, pia tungo lazima ilete maana. Kwa mantiki hiyo kuna uhusiano usio na mashaka kati ya sintaksia na semantiki kwa sababu mpangilio sahihi wa maneno katika sentensi ndiyo huleta maana na bila mpangilio sahihi wa maneno maana hupotea.

 

.Hitimisho;

            Kwa ujumla sintaksia kama tawi mojawapo la isimu linauhusiano wa moja kwa moja na matawi mengine kwani haiwezi kutenganishwa na vitengo vingine vya lugha kutokana na uhusiano mkubwa uliopo baina ya vitengo hivi. Hutegemeana na kuathiriana kwa kiasi kikubwa, mfano huwezi kupata mofolojia bila kupitia ngazi ya fonolojia na pai huwezi kuwa na ngazi ya sintaksia bila kupitia ngazi ya fonolojia na mofolojia lakini vitengo vyote hivi hutawaliwa na kitengo cha semantiki ili kuleta mawasiliano miongoni mwa wazungumzaji.

                                          

 

 

 

 

 

 

MAREJEO

 

Besha, R.M. (2007). Utangulizi wa Lugha na Isimu. Dar es Salaam: Mackmillan Aidan

Habwe, J na P. Karanja (2004). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

International Law

KATIBA YA KIKUNDI